This archive report was first published on 4 October 2019.
Upasuaji wa maiti wa Tob Cohen, mfanyabiashara wa Kiholanzi, umefichua kuwa alifariki baada ya kupigwa na kifaa butu mara kadhaa kwenye mwili wake.
Alipatikana maiti yake ndani ya tanki la ardhini Septemba 13, na upasuaji ulifanywa kwa mwili wake Jumatano, Septemba 18.
Uchunguzi wa maiti ulionesha kuwa Cohen alifariki baada ya kupigwa na kifaa butu kichwani, na kuwa na majeraha mabaya ya upande wa kulia wa kichwa chake, mbavuni na usoni.
Alhamisi, Oktoba 3, mkewe Sarah Wairimu alikana mashtaka dhidi ya mauaji ya mumewe mbele ya Jaji Stella Mutuku na wakati uo huo kuomba mahakama imwachilie kwa dhamana.
Wairimu, ambaye ni mshukiwa mkuu wa mauaji ya Tob Cohen, inasemekana alimuua Cohen kati ya Julai 19 na 20 akishirikiana na wenzake siku ambayo mfanyabiashara huyo aliripotiwa kupotea.