This archive report was first published on 23 September 2019.
Uchaguzi wa Kibra unakoroga vyama vya ODM na Jubilee baada ya wanasiasa wake kuchukua misimamo tofauti kwenye safari ya kumpata mbunge wa eneo hilo.
Wabunge ndani ya Jubilee wamekerwa na hatua ya mbunge mteule wa chama hicho Maina Kamanda kuamua kumpigia debe mgombea wa ODM Imran Okoth ilhali kuna mgombea wa Jubilee.
Mbunge wa Siria John Waluke amesema Maina Kamanda ni lazima atimuliwe chamani kwa kukaidi Rais Uhuru Kenyatta.
Waluke alisema Kamanda hawezi kukaidi chama ambacho kilimteua kwenye bunge na kufanyia kampeni mpinzani wao.
"Kamanda ni mbunge wa kuteuliwa. Ni lazima aheshimu serikali ambayo ilimteua na rais akisema twende hivi, ni lazima atii," Waluke alisema.
Waluke aliongeza, "Rais hawezi sema tumuunge mkono Mariga naye Kamanda aende kumuunga mtu mwingine mkono, hiyo ni kupinga rais."
Ndani ya ODM, mbunge wa Malindi naye Aisha Jumwa aliyechaguliwa kwa tiketi ya ODM alisema Kibra ni Mariga tosha.
Aliwataka viongozi kina mama kuhakikisha wanampigia debe Mariga ili ambwage mgombea wa ODM.