This archive report was first published on 4 November 2021.
Published on November 4, 2021
Maskini jeuri wakataa chakula kwa sababu ya siasa ¶
Wakazi wa eneo la Ganze, Kaunti ya Kilifi, walisusia chakula cha msaada walichopelekewa na Gavana Amason Kingi kutokana na mizozo ya kisiasa.
Ubishani ulikuwa umeibuka kati ya wafuasi wa Bw Kingi wanaounga mkono chama anachohusishwa nacho cha Pamoja African Alliance (PAA) na wale wa ODM katika hafla ya uzinduzi wa barabara.
Hafla hiyo ya kuzindua barabara ya Bamba-Ganze-Kilifi iliongozwa na Waziri James Macharia, na ilikuwa imetangulia usambazaji wa chakula cha msaada kutoka kwa serikali ya kaunti.
Wakazi wa eneo hilo ni wale wanaokumbwa na uhaba mkubwa wa chakula na maji kutokana na athari ya kiangazi cha muda mrefu.
Wakazi walikataa chakula cha msaada hilo, na kiongozi wa kikundi cha vijana Ganze, Bw Fikirini Jacobs, alisema kuwa Bw Kingi alikosa kwa kuanza hotuba yake kwa kuambia wananchi amewafaa kwa kuwaletea chakula cha msaada.
Wanachama wa ODM, wakiongozwa na Seneta wa Kilifi, Bw Stewart Madzayo, walimkashifu gavana kwa kutaka kugeuza hafla muhimu kuwa ya kupigia debe chama chake cha PAA.