This archive report was first published on 16 August 2019.
Seneta Susan Kihika amejitokeza na kuzungumzia mtafaruku kati yake na maafisa wa usalama wa Rais Uhuru Kenyatta baada ya kanda ya video iliyosabaa kwenye mtandao ikionyesha maafisa hao wa usalama wakirushiana maneno na seneta huyo.
Seneta Kihika ameelezea kilichosababisha mzozo na maafisa wa Rais mjini Nakuru. Kulingana na Kihika, utata ulizuka baada ya afisa mmoja wa kitengo hicho cha usalama wa rais kujaribu kumtoa kwenye foleni ya viongozi waliokuwa wamlaki Rais Kenyatta.
‘Afisa mmoja mwanaume alikuja na kunirusha huku akitaka kunitoa kwenye foleni hiyo, ndio utata ukazuka kati yetu kabla ya afisa wa kike kuja kutuliza hali,’ Kihika aliambia gazeti la SDE.
Maafisa hao wa usalama wa rais walikuwa wametoa onyo kwa MaMCAs wote wasikae kwenye foleni ya viongozi waliokuwa wamkaribishe Rais Kenyatta. Walipomuona Kihika, wakadhani ni MCA amedinda kutii agizo lao.
‘MaMCAs walitii agizo hilo na wakarudi nyuma....lakini maafisa hao waliporudi na kumpata seneta, walifikiri ni MCA na mmoja wa maafisa akamfokea na kumrusha,’ Mbunge wa Njoro Charity Kathambi alisema.